KIPIGO cha mabao 3-0 walichokipata Yanga kutoka kwa Mtibwa Sugar kimewaacha mashabiki wao njia panda kuhusu ubora wa safu ya ulinzi ya timu hiyo iliyoruhusu mabao 9 katika mechi 13 hadi sasa.
Yanga ambayo msimu huu iliwasajili mabeki Kelvin Yondani (Simba), Mbuyu Twite (APR), David Luhende (Kagera Sugar) na Juma Abdul (Mtibwa Sugar) ilionekana kuwa ni moja ya timu yenye ngome imara zaidi baada ya kuruhusu mabao manne tu kwenye mashindano ya Kombe la Kagame.
Safu hiyo ya ulinzi ya Yanga inayoongozwa na nahodha Nadir Haroub, Yondani, Twite, Abdul na Luhende Jumatano ilionekana kuwa chochoro mbele ya washambuliaji wa Mtibwa Sugar, Hussein Javu na Dickson Daud.
Kipigo cha mabao 3-0 walichokipata Yanga kiwewashtua mashabiki pamoja na kocha wao Mbelgiji Tom Saintfiet aliyeahidi kulitafutia ufumbuzi suala hilo haraka.
Mashabiki wa Yanga kwa nyakati tofauti waliwalaumu mabeki hao kwa kufanya makosa yaliyowapa nafasi washambuliaji wa Mtibwa Sugar kupata mabao matatu huku mawili yakipachikwa nyavuni na Javu na moja likifungwa na Daud.
Kocha wa Yanga, Saintfiet hata hivyo amewaomba radhi mashabiki wa timu yake na kuahidi kurekebisha haraka mapungufu ya kikosi chake.
Saintfiet alisema kuwa kitendo cha kupoteza mchezo tena kwa kipigo kikubwa kama hicho kimemuumiza na kumkosesha raha kwa vile mazingira ya mchezo yalikuwa na nafasi kwa kikosi chake kuibuka na ushindi.
"Najua mashabiki wetu wameumizwa sana na matokeo haya na wanayo haki la kulalamika kwakuwa faraja yao ni kuona timu inashinda na siyo vingenevyo, lakini niseme kwamba hata mimi nimeumia na ninachoweza kusema naomba watusaheme,"alisema Saintfiet.
Alisema,"ukweli ni kwamba sisi ndiyo tulikuwa na kila sababu ya kushinda, tulitengeneza nafasi nane hatukuitumia hata moja kufunga, tukapata penati pia tukakosa, wenzetu walitengeneza nafasi nne wakapata mabao matatu hii inaonyesha hatukuwa makini."
Saintfiet alisema,"tunatakiwa kujitazama upya, tukiendelea kuangalia matokeo mazuri ya siku haitatusaidia, yaani umakini haupo kabisa na hii ni kutokana na kila mchezaji kujiona yeye nyota, angalia kama lile goli la pili lilikuwa la kizembe kabisa lakini tulishindwa kulizuia."
Kocha huyo alisema kuwa ikiwa wachezaji wake hawatabadilika na kutambua wajibu wao wanapokuwa uwanjani, itakuwa vigumu kufikia malengo waliyojiwekea ya kuhakikisha ubingwa unarejea mikononi mwao.
Naye mshambuliaji Hamis Kiiza aliwaomba radhi mashabiki na kuwataka kuwa na subira kwa kuwa ligi ndiyo kwanza imeanza.
Kiiza alisema anaomba radhi kwa kukosa penalti pamoja na kupoteza mchezo huo, lakini siyo sababu ya kukata tamaa bali wawe kitu kimoja wakati huu timu inapohitaji umakini zaidi na ushirikiano baina yao na viongozi wao.
Shabiki Hassan Omari akizungumzia pambano la Yanga na Mtibwa alisema," ule ni uzembe wa mabeki wetu kwani ukiangalia bao la kwanza mfungaji alikuwa peke yake hakubugudhiwa hata kidogo na hata mabao mawili yaliyofungwa na Javu ni makosa yao wenyewe walinzi hauwezi kumlaumu kipa kabisa.”
Naye Jackson Tesha alisema," Yanga walibweteka na kuidharau Mtibwa Sugar na walikuja hapa kuchukua pointi kirahisi."
Tesha alisema pamoja na uzembe wa wachezaji, lakini kocha Tom Saintfiet alifanya makosa kwa kuchezesha wachezaji kwenye nafasi ambazo sio zao za kila siku.
"Kitendo cha Mbuyu Twite kucheza kama beki namba tatu badala ya namba nne na tano kilimfanya Mkongo huyo kushindwa kucheza kwa kiwango chake,"alisema Tesha.
Katika hatua nyingine uongozi wa Yanga unatarajia kukutana leo na benchi la ufundi la timu hiyo kwa ajili ya kujadili matokeo mabovu ya timu yao kabla ya kuivaa JKT Ruvu kesho kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Imeandaliwa na Juma Mtanda, Morogoro na Sosthenes Nyoni, Jessca Nangawe.