Quantcast
Channel: Tanzania Sports News, Sports News, Tanzania Sports, Tanzania News, Sports Tanzania.
Viewing all 166 articles
Browse latest View live

Azam yaipania Polisi

$
0
0
Kalunde Jamal
KOCHA wa Azam, Boris Bunjak amesema anakwenda Morogoro kuchukua pointi tatu kutoka kwa Polisi Moro ili kuendelea kukaa vizuri katika msimamo wa Ligi Kuu.

Azam inashikilia nafasi ya pili katika msimamo wa Ligi Kuu Bara ikiwa na pointi 13 ikiwa nyuma  ya Simba kwa pointi tatu.

Bunjak alisema anataka washambuliaji wake waongeze juhudi na kufunga mabao zaidi kwani hafurahishwi na ushindi wa mabao machache.

Alisema wachezaji wake wanacheza vizuri na wameshinda mechi nyingi, lakini anataka wakipata nafasi ya kushinda washinde mabao mengi ili wawe kwenye nafasi nzuri zaidi ya kukaa kileleni kwa muda mrefu.

"Nawafundisha wachezaji wangu zaidi kufunga ili wazidi kuwa na uelewa wa kufunga na tukishinda iwe ni ushindi wa mabao mengi  kuliko ushindi wa mabao machache ingawa pointi tatu zinabaki zile zile,"alisema Bunjak.

"Kushinda mchezo wa Jumamosi ni muhimu, ili tuweke hai nia yetu ya kutwaa taji la Ligi Kuu msimu huu baada ya kushindwa kufanya vizuri msimu uliopita," alisema Bunjak.

Azam iliondoka jana mchana kuelekea Morogoro, tayari kwa mchezo huo dhidi ya wenyeji Polisi Moro, kwenye Uwanja wa Jamhuri, Morogoro.

Reddís Miss Tanzania kumsaka Top Model leo

$
0
0
Mwandishi Wetu
WAREMBO wanaoshiriki Reddís Miss Tanzania leo usiku wanatarajiwa kupanda jukwaani kumsaka Miss Top Model, katika shindano linalotarajiwa kufanyika hoteli ya Naura Spring, jijini Arusha.
 
Mshindi wa taji hilo anaingia moja kwa moja kwenye16 bora ya Reddís Miss Tanzania, shindano linalotarajiwa kufanyika Novemba 3, mwaka huu.
 
Tayari Miss Mbulu, Lucy Stephano amefuzu kwa hatua hiyo baada ya kufanikiwa kutwaa taji la Miss Photogenic, lililofanyika Monduli mwishoni mwa wiki.
 
Akizungumza na gazeti hili mjini hapa jana, Afisa Habari wa Kamati ya Miss Tanzania, Haidan Ricco alisema maandalizi yote yamekamilika na kilichobaki ni warembo hao kuonyesha ubabe jukwaani.
 
ìWarembo wote wako sawa na wamejiandaa vema kuhakikisha wanatoa upinzani mkubwa, naamini mashabiki watakaohudhuria watapata burudani ya aina yake,î alisema.
 
Ricco alisema, baada ya shindano hilo warembo wote wanatarajiwa kuondoka mjini hapa kesho asubuhi kuelekea Tanga kwa ajili ya kutembelea mapango ya Amboni, kabla ya kurejea Dar es Salaam.
 
Warembo wapatao 30 wanawania taji la Reddís Miss Tanzania, ambalo kwa sasa linadhaminiwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kupitia kinywaji chake cha Reddís Original.

Magongo, riadha kumuenzi Nyerere

$
0
0
Fina Lyimo, Moshi na Erick Sawe
MSHINDANO ya mpira wa magongo ya kumwenzi Baba wa taifa mwalimu Julias Nyerere yameanza rasmi kutimua vumbi jana kwenye Viwanja vya Sikh klabu ya mjini Moshi mkoani Kilimanjaro.

Mashindano hayo yameshirikisha timu 6, kutoka mikoa mbalimbali ambazo ni Moshi Khalsa, Magereza, Arusha Twiga,  Zanzibar, Dar  Khalsa na Kili Vijana.

Akifungua mashindano hayo Mkuu wa wilaya ya Moshi, Dk. Ibrahim Msengi aliwataka vijana kutumia michezo  kama ajira na kuwaomba kuhubiri amani, umoja na mshikamani kama alivyokuwa baba wa taifa.

ìMashindano haya yasiishie tu viwanjani  bali yatumike kama sehemu ya kutangaza amani upendo pamoja na kutangaza utalii ndani na nje ya nchi,î alisema Dk. Msengi.

Kwa upande wake mratibu wa michezo hiyo Indejeet Rehal, alisema mashindano hayo yalianza miaka minne iliyopita kwa lengo la kumuenzi baba wa taifa.

Rehal alisema kila mwaka timu zinaongezeka na kuwataka wajitikeze kuanzisha timu za michezo wa magongo ili iweze kuzoeleka ndani ya jamii.

Wakati huohuo; Chama cha Riadha Tanzania (RT) kimeandaa Mashindano ya mbio za Riadha za kumuenzi  Baba wa Taifa Julias Nyerere zitakazofanyika Oktoba 14.

Katibu wa Chama cha Riadha Mkoa wa Dar es salaam Kapteni Mustafu Lucas Nkungu alisema kauli mbiu ya mashindano hayo ni Watanzania kupendana na kudumisha moja.

Alisema "Baba wa Taifa aliacha kazi ya Ualimu na kuwaunganisha Watanganyika katika kudai Uhuru na aliwaunganisha makabila yote Tanzania kuongea lugha ya Kiswahili na Azimio la Arusha."

Mashindano hayo yanadhaminiwa na Lotary Club kwa  lengo la kupata fedha za kumalizia ujenzi wa jengo la wodi ya saratani ya watoto katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili linalotarajiwa kumalizika mwezi Machi  mwakani.

Kutakuwa na matembezi ya hiari kwa km 9 kuanzia Golden Tulip Hotel na kuishia Police Officers Mess.

Mgeni rasmi atakuwa ni Rais wa awamu ya pili Ali Hassan Mwinyi na mikoa yote inategemea kushiriki pamoja na Zanzibar, Uganda, Rwanda na Burundi.

Brazil yaifanyia kitu mbaya Iraq

$
0
0

MALMO, Sweden
KAKA aling'ara usiku wa kuamkia jana katika siku yake ya kwanza kuichezea timu ya taifa ya Brazil baada ya kuwa nje kwa miaka miaka miwili, pale miamba hiyo ya soka walipoitia 'adabu' Iraq kwa kipigo cha mabao 6-0 katika mechi ya kirafiki ya kimataifa iliyochezwa kwenye mji wa Malmo, Sweden.

Kiungo huyo wa Real Madrid alikuwa akicheza mechi yake ya kwanza ya kimataifa kwa Brazil tangu alipoichezea mara ya mwisho kwenye fainali za Kombe la Dunia nchini Afrika Kusini mwaka 2010.
Alicheza vizuri kwenye mchezo huo na kufunga bao la tatu akimalizia pasi ya mchezaji wa Chelsea ya England, Oscar.

Hulk aliongeza bao la nne, huku Neymar na Lucas na kila mmoja akipachika bao katika mechi hiyo ambayo sehemu kubwa ilikuwa ya upande mmoja.

Iraq kwa sasa inafundishwa na mchezaji wa zamani wa kimataifa wa Brazil, Zico.
Brazil ilitawala mchezo kwa kiasi kikubwa, huku Oscar akitangulia kufunga bao katika dakika ya 21 akimalizia pasi ya Neymar.

Aliongeza bao lingine baada ya kushirikiana vizuri na Kaka na Neymar.
Kipa wa Iraq Sabri Noor alikuwa imara langoni na bila jitihada zake, Brazil ingeweza kuondoka na mabao mengi zaidi kwenye mchezo huo.

Aliokoa mpira wa kichwa uliopigwa jirani na lango kutoka kwa David Luiz, kisha akafanya hivyo tena kwa kuokoa mashuti ya mwendo mrefu kutoka kwa Kaka na Hulk.

Kikosi cha kocha Mano Menezes kilionyesha uwezo mkubwa, huku pasipo chembe ya mashaka Kaka alionyesha kiwango kizuri na kustahili uwapo wake kwenye kikosi hicho cha Brazil.

Kaka mchezaji bora wa Fifa mwaka 2007 FIFA na mshindi wa tuzo ya Ballon d'Or, aliwapiga chenga mabeki wawili na kumfunga kirahisi kipa Noor.

Muda mfupi baadaye, Hulk aliipeleka mbele Brazil kwa kufunga bao lingine baada ya juhudi binafsi.
"Alicheza vizuri na kusaidia ushindi kwa pasi za uhakika, na kisha yeye mwenyewe kufunga. Kama ataendelea hivi atakuwa mchezaji mzuri," alisema Oscar.

"Nimefurahishwa jinsi tulivyocheza, bao langu nililofunga limenipa furaha zaidi na kuamsha moyo wa kucheza upya kwa ajili ya nchi yangu," alisema Kaka.

Azam yazitaka Yanga, Simba Chamazi

$
0
0
Jessca Nangawe
KLABU ya Azam imeliandikia barua Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kuomba mechi zake za nyumbani dhidi ya Yanga na Simba kuchezwa kwenye uwanja wao wa Azam Complex uliopo Chamazi badala ya Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Ofisa Habari wa TFF, Boniface Wambura alisema jana kuwa wamepokea maombi kutoka kwa uongozi wa Azam ambao unataka kutumia uwanja wao kwa mechi zao za nyumbani kwani una uwezo wa kumudu kuingiza mashabiki wa timu hizo kwa wakati mmoja.

Wambura alisema wao kama wasimamizi wa ligi hiyo wamepokea maombi hayo na yatatolewa ufafanuzi leo na kamati ya ligi ambayo itakutana katika kikao cha pamoja.

Alisema kuwa klabu ya Azam ina haki ya kutumia uwanja wao wa nyumbani katika mechi zake za nyumbani kutokana na kumiliki uwanja wao ambao una uwezo wa kuingiza mashabiki wengi kwa wakati mmoja.

"Tumepokea barua ya maombi kutoka uongozi wa klabu ya Azam ambao unataka kutumia uwanja wao katika mechi zao za nyumbani  badala ya kutumia uwanja wa Taifa kama ilivyokuwa awali, huku wakisisitiza wana kila sababu ya kufanya hivyo kutokana na uwanja wao kuwa na uwezo wa kubeba mashabiki wengi kwa wakati mmoja,"alisema Wambura.

Nayo klabu ya Ruvu Shooting imeomba mechi yake ya ugenini dhidi ya Yanga ya Oktoba 20 mwaka huu ichezwe Uwanja wa Taifa badala ya Uwanja wa Azam Complex.

Kamati ya ligi kuzijadili Yanga, Lyon

$
0
0
Clara Alphonce
KAMATI ya Ligi Kuu Tanzania Bara inatarajia kukutana leo kujadili mambo mbalimbali likiwamo suala la Yanga na African Lyon kushindwa kuvaa nembo ya mdhamini wa ligi hiyo katika mechi zao.

Yanga waligomea kuvaa jezi za mdhamini wa ligi kampuni ya Vodacom ambazo zina nembo nyekundu kwa madai kuwa siyo rangi yao na wameendelea kuvaa jezi zenye nembo ya mdhamini, lakini zenye rangi nyeusi wakati kanuni haiwaruhusu kufanya hivyo.

Hata hivyo kampuni ya Vodacom imekwishaonyesha nia ya dhati ya kutaka kuongea na Yanga kwa ajili ya kumaliza suala mapema kama walivyotakiwa na Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Leodegar Tenga.

Ofisa Habari wa TFF, Boniface Wambura alisema kuwa kamati hiyo ya ligi pia inakutana leo kuongelea ratiba ya ligi ambayo inatakiwa kufanyiwa mabadiliko kidogo.

Alisema kuwa kuna baadhi ya mechi zinatakiwa kufanyiwa marekebisho kama mechi ya Yanga na Ruvu Shooting ambayo ratiba inaonyesha inatakiwa kuchezwa kwenye Uwanja Azam Complex Oktoba 20.

Wambura alisema timu ya Ruvu Shooting imeomba mechi yake hiyo ya ugenini ya Oktoba 20 mwaka huu dhidi ya Yanga ichezwe Uwanja wa Taifa badala ya Uwanja wa Azam Complex.

Alisema maombi hayo yatajadiliwa na kikao cha Kamati ya Ligi kitakachokaa leo na kutoa uamuzi kuhusu maombi hayo.

Coastal, Polisi kuzitibulia Simba, Azam leo?

$
0
0
Calvin Kiwia
VINARA wa Ligi Kuu, Simba na Azam leo watakuwa wakisaka kuendeleza wimbi lao la ushindi wakati watakapozikabili Coastal Union na Polisi Morogoro.

Simba watakuwa wageni wa Coastal Union ya Tanga kwenye Uwanja wa Mkwakwani wakijua wazi kufungwa mchezo huo ni kuikaribisha kileleni Azam wanaocheza dhidi ya vibonde wa ligi hiyo, Polisi Moro kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro.

Mabingwa hao watetezi Simba na Azam FC ndizo timu pekee ambazo kwenye ligi hazijapoteza mchezo wowote mpaka sasa.

Simba watakuwa wakicheza mechi yao ya kwanza nje ya Dar es Salaam msimu huu baada ya kucheza michezo sita ikiwa katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na katika michezo hiyo imeshinda mara tano na kutoka sare moja dhidi ya Yanga na kujikita kileleni mwa msimamo kwa kufikisha pointi 16.

Azam inashikilia nafasi ya pili ikiwa imejikusanyia pointi 13 baada ya kucheza mechi tano.

Vinara wa ligi Simba wamefunga mabao 14 kwenye ligi katika mechi sita walizocheza na kuruhusu mabao manne tu kugusa nyavu zake.

Wapinzani wao Coastal Union waliofanya usajili mkubwa, bado hawajawa kwenye kiwango kizuri baada ya kushinda mechi mbili tu kati ya sita kwa kuzifunga Kagera Sugar na Mgambo JKT huku ikitoka sare tatu na kupoteza mechi moja dhidi ya Ruvu Shooting.
 
Wagosi hao ambao ni mabingwa wa Ligi Kuu mwaka 1988, msimu uliopita waligawa pointi zote sita kwa Simba, huku marehemu Patrick Mafisango akifunga bao pekee kwenye Uwanja wa Mkwakwani mkoani Tanga na Simba kuibuka na ushindi wa bao 1-0.

Hata hivyo, viongozi na wachezaji wa timu hiyo walimlalamikia mwamuzi wa mchezo huo wakidai mpira haukuvuka mstari wa goli.

Nyota wa Coastal Union wanaotegemewa kuisumbua Simba leo ni kiungo Mkenya Jerry Santo, Juma Jabu, Nsa Job, Pius Kisambale, Razack Khalfan, Seleman Khassim 'Selembe' na kipa Jackson Chove.

TAMBO ZA MAKOCHA
Kocha wa Simba, Milovan Cirkovic alisema pambano litakuwa gumu, lakini wamejizatiti vilivyo kuendeleza rekodi ya ushindi.

"Nafikiri Coastal ni timu bora ukiziacha Yanga, Azam na Mtibwa. Imesajili vizuri msimu huu. Naamini mchezo utakuwa mgumu na ushindani wa hali ya juu," alisema Cirkovic ambaye ni raia wa Serbia.

Mserbia huyo alisema,"Ni mchezo wetu wa kwanza kucheza nje ya Dar es Salaam katika Ligi Kuu msimu huu. Siwezi kusema kwamba hiyo ni sababu yetu ya kushindwa kuendeleza ushindi,  tumejizatiti kwa kila hali kupata pointi zote tatu na kuzidi kupaa kileleni."

Naye kocha mpya wa Coastal Union, Hemed Morocco aliyevaa mikoba ya Juma Mgunda aliyejiuzulu kwa shinikizo la wanachama na mashabiki wa timu hiyo alisema amefanya masahihisho kidogo kwenye kikosi chake baada ya kupoteza mchezo uliopita dhidi ya Ruvu Shooting na kufungwa mabao 2-0.

"Nafikiri kuna kasoro nilizoziona kwenye mchezo uliopita dhidi ya  Ruvu nimejaribu kuzifanyia marekebisho ili kuhakikisha tunashinda pambano letu na Simba,"alisema Morocco.

Alisema,"Simba ni timu nzuri na hivi sasa ipo kwenye kiwango kizuri cha soka isipokuwa tumejipanga kukabiliana nayo kwa kila hali."

MICHEZO MINGINE
Azam iliyozidiwa pointi tatu na vinara Simba, itakuwa ikijaribu kuziba pengo hilo wakati itakapovaana na Polisi Moro kwenye Uwanja Jamhuri mjini Morogoro.

Mtibwa Sugar ikiwa kwenye Uwanja wake wa Manungu, yenyewe itawaalika vibonde Mgambo JKT ya Handeni Tanga.   

Wakati Tanzania Prisons itakuwa mwenyeji Oljoro JKT kwenye Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya.

Nayo Ruvu Shooting baada ya kuichapa Coastal Union mabao 2-0,  itavaana na African Lyon kwenye Uwanja wa Mabatini mkoani Pwani.

Okwi, Kiiza waivaa Zambia

$
0
0
Mwandishi Wetu
WASHAMBULIAJI Emmanuel Okwi na Hamisi Kiiza wataweka kando tofauti zao za Usimba na Uyanga wakati watakapoiongoza Uganda kusaka tiketi ya kufuzu kushiriki Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika dhidi ya mabingwa watetezi Zambia leo kwenye Uwanja wa Namboole, Kampala.

Okwi na Kiiza leo watakuwa na jukumu moja la kuhakikisha Uganda inashinda mechi na kufuzu kushiriki Fainali za Afrika kwa mara ya kwanza baada ya kushindwa kufanya hivyo kwa miaka 34.

Uganda wanahitaji ushindi wa mabao 2-0 ili kujihakikishia nafasi hiyo baada ya kuzikosa fainali za 2012 kutokana na kulazimishwa sare 0-0 na Kenya kwenye mchezo wa mwisho.

Mchezo huu wa Uganda dhidi ya Zambia umevuta hisia za mashabiki wengi wanaotaka kuona bingwa mtetezi Zambia akiaibika na kuliacha taji hilo mapema.

Katika kuhakikisha wanaepuka aibu hiyo tayari Serikali ya Zambia imetangaza dau nono la dola 5000 sawa (Sh7,765,350) kwa kila mchezaji endapo wataifunga Uganda.  

Zambia wataingia uwanjani wakiwa na rekodi ya kushinda michezo 13, kutoka sare saba na kufungwa 11 kwenye michezo yake ya kimataifa iliyocheza dhidi ya Uganda.

ETO'O KIBARUANI
Mshambuliaji Samuel Eto'o amereja Cameroon kwa lengo la kuhakikisha wanaepuka janga la kuondolewa kwenye Kombe la Mataifa ya Afrika na timu mdogo ya Cape Verde.

Katika mechi ya kwanza iliyozikutanisha timu hizo, Cameroon ilichapwa mabao 2-0.

Mbali ya Cape Verde, pia Jamhuri ya Afrika Kati watakuwa wakisaka kufuzu kwa mara ya kwanza kushiriki fainali hizo.

Eto'o alisema,"Kwa pamoja na tukiweka kando tofauti zetu na msaada wa Mungu kwa hakika Cameroon itafuzu bila ya shaka."

Jamhuri ya Afrika  ya Kati iliyoruka kutoka nafasi ya 200 kwenye viwango vya ubora wa FIFA mwaka 2009 hadi 49 mwezi uliopita, watakuwa wenyeji wa Burkina Faso. Katika mechi ya kwanza Jamhuri ya Afrika ya Kati walifungwa bao 1-0.

Ivory Coast ya Didier Drogba itakuwa na kibarua kigumu mbele ya Senegal ya Demba Ba na Papiss Cisse. Katika mechi ya kwanza Ivory Coast ilishinda 4-2.

Ethiopia watajiuliza upya kwa Sudan baada ya mchezo wa kwanza kuchapwa 5-3 huku Algeria, DR Congo, Ghana, Mali, Nigeria na Tunisia ndio timu pekee zilizojiweka kwenye mazingira mazuri ya kufuzu.

Ratiba
Leo
Malawi v Ghana
Uganda v Zambia
Botswana v Mali
Nigeria v Liberia
Tunisia v Sierra Leone
Senegal v Ivory Coast
Morocco v Msumbiji

Kesho
Ethiopia v Sudan
Cameroon v Cape Verde
Angola v Zimbabwe
Niger v Guinea
Togo v Gabon
Guinea ya Ikweta v DR Congo
Burkina Faso v Jamhuri ya Afrika ya Kati
Algeria v Libya

Kipa Polisi aomba radhi

$
0
0

Mwandishi Wetu
KIPA wa Polisi Morogoro, Manzi Manzi ameowaomba msamaha mashabiki wa timu yake kufuatia kipigo cha bao 1-0 ilichokipata kutoka kwa Azam mwishoni mwa wiki.

Baadhi ya mashabiki walioshuhudia pambano hilo lililofanyika kwenye Uwanja wa Jamhuri walisikika wakimlaumu Manzi kwa uzembe na kusababisha kipigo hicho.

Manzi alisema haikuwa kusudi kama mashabiki wengi wanavyodai na baadhi ya viongozi kumlaumu kwa kitendo kile ilikuwa ni sehemu ya mchezo na aliamini kusingetokea madhara yoyote.

Manzi alifafanuwa kuwa hakuna haja ya malumbano bali aliwataka mashabiki kutulia na kumsamehe na wawe kitu kimoja na timu kuelekea kwenye dhidi ya JKT Ruvu.

"Nawaomba radhi mashabiki wa timu yetu na wadau wa soka wa Mkoa huu na Tanzania nzima kwa ujumla kwa makosa yangu, lakini kwa upande wangu sikuwa na nia mbaya ya kuihujumu timu"alisema Manzi.

Lyanga awaita Yanga

$
0
0
Mwandishi Wetu
WINGA wa Coastal Union, Danny Lyanga amesema yuko tayari kujiunga na Yanga au klabu yoyote inayomtaka baada ya kumaliza kwa mkataba wake.

Lyanga alisema awali alishindwa kutoondoka Coastal kutokana na kufungwa na mkataba, lakini sasa mkataba huo unaelekea ukiongoni hivyo timu yeyote ikiwemo Yanga inaweza  kufanya mazungumzo naye.

"Kweli Yanga wamenifuata zaidi ya mara tatu wakitaka kunisajili,  lakini nishindwa kutokana na kubanwa na mkataba wangu."alisema Lyanga na kuongeza:

"Mkataba wangu unakaribia kumalizika na kama unavyojua kila mtu ana malengo yake katika maisha na katika kazi maslai ndiyo jambo muhimu hivyo tutaafikiana hakuna tatizo nitaondoka na kujaribu bahati kwingine."

Tchetche ligi ngumu

$
0
0
Kalunde Jamal
MSHAMBULIAJI wa Azam, Kipre Tchetche amesema msimu huu ligi imekuwa ngumu na ushindani ni mkubwa kwa timu zote.Tchetche alisema ushindani huo unatokana na timu zote kufanya maandalizi ya uhakika tofauti na ilivyokuwa msimu uliopita.

Akizungumzia mechi yao dhidi ya Prisons hapo kesho, Tchetche alisema anategemea ushindani mkubwa kutokana na ubora wa timu hiyo ikiwa kwenye uwanja wake wa nyumbani.

"Najua Prisons ni timu ngumu kufungika, lakini nafahamu udhaifu wao baada ya kucheza nao mara mbili katika mechi za kirafiki nitahakikisha nadhani hiyo itatusaidia kupata pointi tatu,"alisema mpachika mabao huyo.

Naye kocha Boris Bunjak alisema kikosi chake kipo tayari kimwili na kiakili tayari kwa kuisambaratisha Prisons.

"Unapocheza nje ya uwanja wako utarajie mchezo mgumu, lakini katika soka sisi tunasema yule mwenye uwezo ndiye atakayeshinda, naamini Azam iko katika fursa nzuri zaidi ya kuondoka na pointi tatu,"alisema Bunjak.

Azam inakamata nafasi ya pili na pointi zake 16 wakiwa nyuma kwa pointi moja kwa vinara Simba kabla ya michezo yao ya kesho.

Milovan ajitetea kumpanga Ochieng

$
0
0
Calvin Kiwia
KOCHA wa Simba, Milovan Cirkovic ameweka bayana sababu zilizomfanya ampange beki Paschal Ochieng badala la Juma Nyosso kwenye pambano la Ligi Kuu dhidi ya Coastal Union.

Mechi dhidi ya Wagosi wa Kaya, Coastal ilikuwa ya  kwanza kwa Mkenya huyo aliyejiunga na Simba msimu huu akitokea AFC Leopard.

Kabla ya pambano dhidi ya Coastal, Cirkovic alikuwa akiwachezesha Shomari Kapombe na Juma Nyosso kama mabeki wa kati huku akimwacha Ochieng kama mchezaji wa akiba.

Akizungumza na  Mwananchi, Cirkovic alisema alimpanga Ochieng kwa lengo la  kutazama maendeleo yake baada ya kumpa maagizo ya kuhakikisha anafanya mazoezi magumu kupunguza uzito na kurejesha kasi yake Uwanjani.

"Nafikiri Ochieng (Paschal) sasa ameanza kuimarika kwani ameonyesha utofauti mkubwa na aliovyokuwa awali." alisema Cirkovic na kuongeza:

"Ni mchezo wake wa kwanza kucheza kwenye ligi. Nafikiri ameanza kuimarika. Nitampa nafasi mara kwa mara aweze kujiamini na kuzoea mazingira." alisema Cirkovic.

"Nafikiri ndio mchezo wangu wa kwanza kucheza kwenye ligi. Binafsi najisikia furaha kuona sasa mwalimu ameanza kujenga imani nami na kunipa nafasi yakucheza." alisema Ochieng.

Hispania, Ufaransa haponi mtu leo

$
0
0
MADRID, Hispania
MBIO za kusaka tiketi ya kucheza Fainali za Kombe la Dunia 2014 nchini Brazil zitaendelea barani Ulaya leo kwa mechi kadhaa, lakini kivutio zaidi kitakuwa mchezo kati ya mabingwa watetezi Hispania dhidi ya Ufaransa.

Ni nadra kwa timu kubwa barani Ulaya kukutana katika hatua ya makundi,  ila safari hii Ufaransa inachukuliwa kama kibonde, jambo linaloifanya mechi ya leo kuwa kivutio.

Ufaransa, bingwa wa dunia mwaka 1998 zama hizo ikiwa na kina Zinedine Zidane, Thierry Henry na wengineo akiwamo kocha wa sasa wa Ufaransa, Didier Deschamps ilifanya vibaya katika fainali zilizopita za mwaka 2010 nchini  Afrika Kusini.

Matokeo hayo yaliisababishia kuondolewa kwenye orodha ya vijogoo Ulaya, hivyo kupangwa kundi moja na Hispania.

Hata hivyo timu hizo, kila moja imeshinda mechi zake mbili za mwanzo huku zikiwa zimeruhusu bao moja kila moja katika nyavu zao.

Nao Romania ambao hawajafuzu kucheza fainali hizo tangu mwaka 1998 imeanza vema mashindano hayo ya kufuzu katika kundi D,  ikizilaza Uturuki, Andorra na Estonia bila kuruhusu bao.

Lakini leo inakutana na Uholanzi inayoundwa na nyota wengi chini ya kocha maarufu Louis van Gaal ambaye ameiwezesha timu hiyo kufunga mabao tisa katika mechi tatu za awali.

Mchezo huo unachukuliwa na wengi kuwa utakuwa wenye ushindani wa aina ya pekee.

Hungary yenye pointi sita katika kundi hilo itakuwa mwenyeji wa Uturuki (yenye pointi tatu) katika mchezo mwingine wa kundi D.

Kundi E, vinara Uswisi ambao wamewahi kufungwa na Luxembourg na Montenegro chini ya kocha Ottmar Hitzfeld aliyechukua mikoba hiyo mwaka 2008 , wataikabili Iceland timu ndogo  ambayo iliishangaza dunia baada ya kuilaza Norway.

Iceland yenye wakazi 320,000 mwaka jana ilifuzu kushiriki fainali za vijana za Ulaya  chini ya miaka 21, jambo  lililomfanya Rais wa Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), Sepp Blatter kuimwagia sifa kuwa inaweza kuwa mfano wa kuigwa na wengine.

Sweden, timu ngumu ina kibarua kigumu dhidi ya Ujerumani, wakati Russia ambayo Ijumaa iliiadhiri Ureno kwa bao 1-0 itakuwa kibaruani dhidi ya Azerbaijan.

Ubelgiji na Croatia zinasaka nafasi ya kukaa kileleni mwa kundi A zikiwa na pointi saba kila moja huku England ikisaka mbinu za kuwakimbia wapinzani wake katika mchezo mwingine dhidi ya Poland.

Italia ambao wameanza vema mashindano hayo ya kufuzu  wanaikabili Denmark ambayo inajivunia nyota kama Zlatan Ibrahimovic na beki Christian Kjaer ambaye ameapa kumzuia Mario Balotelli.

Basena aishitaki Simba CAF

$
0
0
Majuto Omary
ALIYEKUWA kocha mkuu wa Simba, Moses Basena ameliandikia barua Shirikisho la Soka Afrika (CAF) akidai klabu hiyo imlipe dola 72,000 (sawa na sh 112.3 milioni) kwa sababu ya kuvunja naye mkataba.

Akizungumza na Mwananchi kwa njia ya simu kutoka Uganda, Basena ambaye hivi sasa anaifundisha klabu ya Express ya nchini humo alisema kiasi hicho kinaweza kuongezeka kwa sababu hajaorodhesha gharama za madhara aliyoyapata baada ya klabu ya Simba kuvunja naye mkataba.

Basena alisema tayari ameishawaandikia barua CAF na wamemtaarifu watalifanyika kazi suala hilo.Alisema pia amelitaarifu Shirikisho la Soka la Uganda (FUFA) ili kusimamia suala hilo na kufungua kesi katika mahakama ya Tanzania kwa ajili ya kupata haki zake.

Basena alisema kwamba hajafurahia jinsi klabu ya Simba walivyolishughulikia suala la madai ya malipo yake huku akisema walimuambia watalimpa madai yake kupitia kwa mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Simba, Swed Mkwabi, lakini hawajafanya hivyo.

"Nina matumaini kwamba suala hili litamalizwa kwa amani, lakini natambua kuwa viongozi wa Simba walikuwa wakinichezea mchezo mchafu na mimi sikuwa nataka kuwashitaki CAF au kufungua kesi mahakamani, lakini nimechoka ahadi hewa ndiyo maana hivi nimeamua kutafuta njia nyingine za kupigania haki zangu,"alisema Basena.

Alisema kuwa haamini jinsi klabu ya Simba inavyolishughulikia suala la maslahi yake kwa sababu alifanya nao kazi vizuri, lakini anashangaa wamebadilika wakati aliiacha Simba ikiwa juu kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara.Basena ambaye aliinoa Simba kwa miezi saba alisema kwamba klabu ya Simba haikumpa taarifa mapema ya kuvunja naye mkataba na kumchukua kocha anayeinoa Simba hivi sasa Milovan Cirkovic kutoka Serbia.

Tayari Kamati ya Shirikisho la Soka la Tanzania (TFF) inayoshughulikia Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji imesema haikuwa na mkataba wa Basena uliosajiliwa TFF kama kanuni na taratibu zinavyotaka kwa hiyo Simba na Basena ndiyo watakaolimaliza suala hilo.

Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Kamati hiyo ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ya TFF, Alex Mgongolwa, kocha Basena alifanya kazi nchini kinyume cha sheria na alikuwa hana kibali cha kufanya kazi nchini.

Mgongolwa alisema Basena na Simba walikuwa wameingia mkataba bila kufuata sheria.

Simba walivunja mkataba na kocha Basena baada ya kocha huyo kushindwa kuipatia Simba vyeti vyake vya ukocha kama walivyokubaliana. Hata hivyo Basena alipeleka vyeti vyake Simba baadaye wakati tayari Simba ilikuwa imeishaamua kuachana naye na kumchukua kocha Milovan.

Baada ya uongozi wa Simba kupata vyeti vya kocha Basena ulisema kocha huyo aliwadanganya kwa sababu awali aliwaambia kuwa ana shahada ya ukocha, lakini vyeti alivyowapatia Simba vinaonyesha ana diploma.

Msemaji wa FUFA, Rogers Mulindwa akilizungumzia suala hilo alithibitisha kuwa ni kweli Basena amewapa taarifa za madai yake na kuwataarifu CAF.

Mulindwa alisema FUFA inamuunga mkono Basena na tayari kocha Basena amefungua kesi katika mahakama kuu ya Uganda.

Naye Ofisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga alisema kuwa hawana taarifa za Basena kuishitaki Simba katika Shirikisho la Soka Afrika CAF wala mahakamani ila watalishughulikia suala hilo kabla halijafika mbali kwani walikuwa na mkataba na Basena ambao ni baina yao Simba na kocha huyo.

Mintanga huru

$
0
0
James Magai
HATIMAYE Rais wa zamani wa Shirikisho la Ngumi la Tanzania (BFT), Alhaji Shaban Mintanga aliyekuwa akikabiliwa na kesi ya kusafirisha dawa za kulevya, ameachiwa huru baada ya kusota mahabusu kwa miaka minne.Katika kesi hiyo, Mintanga alikuwa akikabiliwa na tuhuma za kula njama na kusafirisha dawa za kulevya zenye uzito wa Kg. 4.8 kutoka Tanzania kwenda nchini Mauritius kwa kuwatumia wachezaji wa timu ya Taifa ya Ngumi za Ridhaa.

Hata hivyo, jana Mintanga aliachiwa huru na Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, bila kujitetea baada ya mahakama kuridhika kuwa hana kesi ya kujibu.

Katika uamuzi wake wa kama mshtakiwa ana kesi ya kujibu au la, Jaji Dk Fauz Twaib alisema kwamba ameridhika kuwa mshtakiwa hana kesi ya kujibu kwa kuwa upande wa mashtaka umeshindwa kuthibitisha mashtaka dhidi yake.

Wakati wa majumuisho ya hoja, Wakili wa Serikali Mkuu (PSA) Fulgence Rweyongeza alidai kuwa upande wa mashtaka umethibitisha mashtaka dhidi ya mshatakiwa na kwamba mshtakiwa ana kesi ya kujibu.

PSA Rweyongeza hata hivyo alidai kuwa ushahidi wao katika kesi hiyo ni wa kimazingira na kwamba ushahidi wa kimazingira ni bora zaidi katika kesi hiyo.

Ushahidi huo wa mazingira ambao upande wa mashtaka uliuegemea ni namba za simu zilizodaiwa kukutwa kwenye tiketi za watu wanaodaiwa kukutwa na dawa hizo nchini Mauritius.

PSA Rweyongeza alidai kuwa shahidi wa kwanza, Christopher Mutabarukwa ambaye alikuwa Makamu wa Rais wa BFT alidai kuwa namba hizo za simu ni namba za mshtakiwa.

Ushahidi mwingine ni ushahidi wa shahidi wa pili wa upande wa mashtaka, Nassoro Michael Irenge aliyekuwa kocha wa timu hiyo wakati wanaenda nchini Mauritius.

Katika ushahidi wake, Irenge alidai kuwa watu waliokamatwa na dawa hizo walitambulishwa kwake na mshtakiwa kuwa wataambatana na timu hiyo kama mashabiki.

Hata hivyo katika uamuzi wake jana, Jaji Dk Twaib alisema kuwa katika kesi hiyo ushahidi wa moja kwa moja ulikuwa ni bora zaidi.

Alisema kuwa inawezakana kuwa mahakama ikamtia hatiani mshtakiwa kwa kutumia ushahidi wa mazingira mahali ambapo ushahidi huo wa mazingira haumgusi mtu mwingine zaidi ya mshtakiwa kuwa ndiye aliyetenda kosa husika.

Jaji Dk Twaib alisema kwamba anakubaliana na hoja za mawakili wa utetezi, Jerome Msemwa, Yassin Membar na Berious Nyasebwa kwamba kati ya mashahidi wote wanne wa Jamhuri, hakuna hata shahidi mmoja aliyetoa ushahidi unaomgusa mshtakiwa kiasi cha kumtaka apande kizimbani kujitetea.

Pia, Jaji Dk Twaib alikubaliana na hoja za utetezi kuhusu udhaifu wa shahidi wa upande wa mashtaka, husasani mkanganyiko wa maelezo ya mashahidi na vielelezo vilivyowasilishwa mahakamani mambo ambayo yanamnufaisha mshtakiwa huyo.

Miongoni mwa udhaifu huo wa ushahidi wa upande wa mashtaka ni pamoja na tofuti ya uzito wa dawa alizokuwa akihusishwa nazo mshtakiwa.

Hoja nyingine ya upande wa utetezi ambayo Jaji Dk Twaib alikubaliana nayo ni kuwa hakuna kielelezo cha dawa hizo kilichowasilishwa mahakamani hapo kama kielelezo, kama Wakili Msemwa alidai kuwa hakuna hata picha ya dawa hizo.

Akizungumzia hoja za mawakili wa utetezi kuwa kama hakuna shahidi hata mmoja aliyeweza kueleza jinsi ambavyo mshtakiwa alihusika katika dawa hizo kwa nini mshatakiwa alazimike kujitetea, Jaji Dk Twaib alisema,ì Sioni sababu ni kwa nini (mshtakiwa ajitetee).î

Jaji Dk Twaib pia alikubaliana na hoja za upande wa utetezi kuwa hakuna ushahidi kuthibitisha kuwa dawa hizo kweli zilikuwa ni  dawa za kulevya kwa kuwa hakuna hati ya uthamini ya dawa hizo iliyoandaliwa  na Kamishna wa Kudhibiti Dawa za Kulevya.

ìHuu ni udhaifu mwingine wa ushahidi wa upande wa mashtaka. Kamishna mwenyewe hakuweza kuziona dawa hizo (zilikuwa zikidaiwa kuwa ni za kulevya), na alishughulikia taarifa za mazungumzo kwenye simu tu,î alisema Jaji Twaib na kuongeza:
ìNina  mashaka kama hii inatosha kuthibitisha kuwapo kwa dawa za kulevya na utendaji wa kosa la kusafirisha dawa za kulevya.î

Akizungumzia mkanganyiko wa uzito wa dawa hizo, Jaji Dk Twaib alisema kwamba kwenye hati ya mashtaka inadaiwa kuwa zilikuwa kilogramu 4.8 wakati kwenye fax (iliyotumwa kutoka Mauritius) inasema kuwa zilikuwa kilogramu 6.

Alisema hakuna shahidi yeyote aliyetoa ushahidi kuhusu asili na uzito wa dawa hizo.

Pia Jaji alizungumzia utata wa ushahidi wa shahidi wa nne mpelelezi wa kesi hiyo, Charles Ulaya ambaye alidai kuwa watuhumiwa wawili wanaoshikiliwa nchini Mauritius walimwambia kuwa walipewa dawa hizo na mtu waliyemtaja kwa jina la Mika na kwamba hawamjui Mintanga.

Pia Jaji alikubaliana na hoja za mawakili wa utetezi Msemwa na Nyasebwa kuwa upande wa mashtaka ulishindwa kueleza mahali na muda ambao mshtakiwa alikula njama za kutenda kosa hilo.

ìKwa matokeo hayo, ninamuona mshtakiwa kuwa hana hatia. Chini ya kifungu cha 293 (1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, ninamuachia huru kwa mashtaka yote yaliyokuwa yakimkabili na anapaswa kuachiwa mara moja isipokuwa kama ataendelea kushikiliwa kisheria kwa makosa mengine,î alisema Jaji Dk Twaib.

Wakizungumzia uamuzi huo, mawakili wa Mintanga walielezea kufurahishwa kwao kwa kuwa wamepambana kwa muda mrefu kuhakikisha haki inatendeka na hatimaye imetendeka.

Msemwa alisema kuwa walikuwa wameiachia mahakama kwani ndio yenye uamuzi wa mwisho na kwamba wanafurahia sana huku Nyasebwa akisema kuwa wameuangusha mbuyu (Jamhuri ya Muungano wa Tanzania).

Matumaini ya Mintanga kuachiwa huru katika hatua hii ya awali ya kutokuwa na kesi ya kujibu yalianza kuchomoza Agosti 29, baada ya Mahakama Kuu kutupilia mbali maombi ya upande wa mashtaka kuongezewa muda wa kuwaita mashahidi wao waliodai kuwa ndio muhimu katika kesi hiyo.

Mashahidi hao ni watanzania watatu waliokuwa katika msafara wa timu hiyo kwenda Mauritius wanaokabiliwa na kesi kama hiyo ya dawa za kulevya walizokamatwa nazo nchini humo na maafisa wawili wa Serikali ya Mauritius.

Kutokana na mashahidi hao kukabiliwa na kesi hiyo nchini Mauritius, kesi ya Mintanga imekuwa ikiahirishwa mara kwa mara kutokana na maombi ya upande wa mashtaka ukiomba kuongezewa muda wa kuwaleta nchini kuja kutoa ushahidi dhidi ya Mintanga bila mafanikio.

Jambo hilo liliwalazimu mawakili wa Mintanga, Berious Nyasebwa kutoka kampuni ya Uwakili ya Member Law Attorneys na Aliko  Mwamanenge wa Kampuni ya Msemwa & Co. Advocates kuiomba  Mahakama itumie mamlaka yake kuilazimisha Jamhuri kufunga ushahidi wake.

Akitoa uamuzi jana Jaji Dk Twaib alitupilia mbali maombi hayo ya Jamhuri na kuamua kufunga ushahidi wa upande wa Jamhuri huku akiagiza pande zote kuwasilisha majumuisho ya hoja iwapo mshtakiwa ana kesi ya kujibu au la.

Katika uamuzi wake Jaji Dk. Twaib alisema kuwa katika kuhakikisha kuwa haki inatendeka kwa pande zote alitoa muda wa kutosha kwa Jamhuri kuwaleta mashahidi wake hao bila mafanikio na kwamba imeonesha kufanya uzembe katika suala hilo.

Alisema kuwa kila mara Jamhuri imekuwa ikiomba ahirisho kwa madai ya kuwaandaa mashahidi wake, jambo ambalo limekuwa likichelewesha mwenendo wa kesi hiyo na hivyo kupoteza muda wa mahakama.

ìHivyo mahakama inatumia mamlaka yake chini ya kifungu cha 264 cha CPA (Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai),îalisema Jaji Dk Twaib na kuamuru pande zote ziwasilishe majumuisho ya hoja kama mshtakiwa ana kesi ya kujibhu au la.

Mitanga alikuwa akidaiwa kushirikiana na watu wengine ambao hawajafikishwa mahakamani hapo, waliokuwa kwenye msafara wa  timu hiyo iliposafiri kwenda kushiriki michezo ya ngumi nchini humo mwaka 2008, ambapo walitiwa mbaroni kwa tuhuma za kuingiza dawa za kulevya nchini humo.

Wanaodaiwa kukamatwa na dawa hizo nchini humo ni pamoja na kocha wa timu hiyo Nassoro Michael Irenge, Bondia Patrick Emilian, Petro Mutagwa na watu wengine wawili waliodaiwa kuwa ni mashabiki Charles Nathaniel na Rajabu Msengwa.

Hata hivyo; Irenge na Emilian walishaachiwa huru na kurejea nchini baada ya kubainika kuwa hawana hatia, lakini bondia Mutagwa na wengine waliodaiwa kuwa ni mashabiki pamoja na mwanamke mmoja raia wa Kenya bado wanashikiliwa mahabusu nchini humo.

Tisa zathibitisha kushiriki Rock City Marathon

$
0
0
Clara Alphonce
MATAIFA tisa yamethibitisha kushiriki mbio za kilomita 21 za Rock City Marathon zinazotarajiwa kufanyika Oktoba 28 kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.

Mratibu wa mbio hizo, Grace Sanga kutoka Kampuni ya Capital Plus International (CPI), waandaji wa mbio hizo za kila mwaka alisema kuwa mialiko katika mbio hizo imeongezwa na sasa wanariadha kutoka mataifa ya Ulaya wanatarajiwa kushiriki.

Alizitaja nchi zilizoalikwa na kuthibitisha kuwa ni Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, DR Congo, Australia, India, Canada na Marekani,  ambapo aliongeza kuwa wanatarajia namba ya washiriki kuongezeka kwa mwaka huu kutokana na maandilizi mazuri.

Tumejitahidi kutuma mialiko ya kushiriki kwa wadau wote wa riadha katika nchi jirani ili waweze kushiriki mbio za Rock City na tunatarajia kupata washiriki wengi zaidi kutoka nje,î alisema Grace.

Mbio hizo za kila mwaka zimegawanyishwa katika makundi matano, na kutakuwa na mbio za kilomita 21 kwa wanawake na wanaume, kilomita tano kwa watu wote, kilomita tatu kwa watu wenye ulemavu, kilomita tatu kwa wazee (miaka 55 na kuendelea) na kilomita mbili kwa watoto umri kati ya miaka saba mpaka kumi.  

Sanga alisema kuwa mbio hizo zinazoonyesha mafanikio makubwa tangu zizinduliwe mwaka 2009 na zinalenga kukuza utalii wa ndani  kupitia michezo kama kauli mbiu yake inavyosema 'tukuze utalii wa ndani kupitia michezo'.

Mashindano ya mwaka huu yamedhaminiwa na Mfuko wa Hifadhi ya Taifa ya Jamii (NSSF), Airtel Tanzania, Geita Gold Mine, Shirika la Ndege la Air Tanzania, Parastal Pension Fund (PPF), African Barrick Gold, New Africa Hotel, Nyanza Bottles, New Mwanza Hotel, TANAPA na Bodi ya Utalii Tanzania (TTB).  

"Mambo yanakamilika na naamini kila kitu kitafanyika kwa wakati," alisema Grace huku akihamasisha mashabiki kumshuhudia msanii Juma Nature na kundi lake la TMK Wanaume atakayetumbuiza wakati wa mashindano hayo.            

Fomu za usajili za mbio hizo zinapatikana kwenye Uwanja wa Nyamagana Jijini Mwanza, Ofisi za Kampuni ya Capital Plus International Ltd zilizopo jengo la ATC ghorofa ya tatu na pia zinapatikana katika blog ya rockcitymarathon.blogspot.com.

Uchaguzi DRFA wasogezwa

$
0
0
Jessca Nangawe
KAMATI ya Uchaguzi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) imeendelea kusababisha uchaguzi wa Chama cha soka Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) kuhairishwa baada ya kamati hiyo kusogeza mbele tarehe ya maamuzi ya kupitia mapingamizi.

Kamati hiyo ya uchaguzi ya TFF inatarajia kukutana kesho.

Awali uchaguzi huo ulipangwa kufanyika Septemba 24, lakini  ulisogezwa mbele tena hadi Oktoba14 kutokana na mkanganyiko wa kanuni, hata hivyo uliahirishwa tena kwa mara nyingine kwa sababu kamati hiyo ya uchaguzi imeshindwa kupitia na kuweka wazi pingamizi zilizotolewa na baadhi ya wanachama wa Chama hicho.

Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah alisema jana kuwa kikao hicho kilichokuwa kifanyike jana kimeahirishwa baada ya wajumbe wanaounda kamati hiyo kushindwa kufika katika kikao hicho.

Uchaguzi wa Chama hicho umeingia katika sura mpya baada ya pingamizi za wagombea waliotakiwa kuondolewa katika kinyang'anyiro hicho kurudishwa huku wanachama waliowasilisha rufaa hizo kudai kuishtaki kamati hiyo mahakamani kwa kukiuka kanuni za uchaguzi.

Taarifa za ndani ambazo Mwananchi ilizipata ni kuwa wagombea waliowekewa pingamizi tayari wamepitishwa na kamati hiyo ya uchaguzi ya TFF inayoongozwa na Deogratius Lyato hali iliyosababisha mpaka sasa kamati kushindwa kuweka wazi waliyoadhimia baada ya kupitia mapingamizi.

"Kilichotokea ni wagombea wote waliowekewa pingamizi wamepitishwa, lakini kamati imekuwa ikishindwa kuweka mambo wazi kwa wanachama na habari tulizozipata ni kwamba wale waliopeleka pingamizi zao wamedai endapo hakutakuwa na majibu ya kuridhisha watakwenda katika ngazi za juu zaidi kutafuta haki zao,"kilisema chanzo hicho.

Yanga, Lyon wadai

$
0
0
Vicky Kimaro
KLABU ya Yanga na African Lyon zimelitaka Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kuwapa mgao wao wa haki za matangazo ya televisheni kutoka Star TV.

Yanga wiki moja iliyopita iliandika barua TFF kutaka maelezo ya kujua Star TV wamenunua haki ya kuonyesha Ligi kwa gharama ya kiasi gani na kutaka mgao wao la sivyo michezo yao isionyeshwe.

Nayo African Lyon jana iliandika barua TFF kutaka kupata mgao wao baada ya mchezo wao dhidi ya Yanga kuonyeshwa kwenye kituo hicho cha televisheni.

Katibu Mkuu wa Yanga, Lawrance Mwalusako alisema, "tumewaandikia barua TFF zaidi ya wiki moja sasa, lakini hakuna majibu yoyote, hakuna chochote kinachoendelea, tunataka mgao wetu na tunataka kuona huo mkataba wa Star Tv."

"Haiwezekani michezo yetu irushwe 'live' halafu sisi hatupati chochote na hatujashirikishwa kwa lolote, kwa kawaida tulikubaliana kila klabu ipewe sh 10 milioni kutokana na haki za televisheni, lakini hakuna chochote kimefanyika mpaka sasa," alisema Mwalusako.

Naye Mkurugenzi wa Lyon, Rahimu Kangezi alisema,"tumeandika barua leo (jana), tumeipelekea TFF tunataka kujua mkataba wa Star Tv na watueleze TFF inaingiaje mkataba bila ya kushirikisha klabu."

"Huu ni mkataba wa pili ambao unaingiwa kienyeji, ule wa Vodacom mpaka leo hatuujui na huu tena hivyo hivyo wakati tulishakubaliana kuwa hakuna kuingia mkataba wowote bila ya kushirikisha klabu,"alisema Kangezi.

Mwananchi ilipomtafuta Mwenyekiti wa kamati ya Ligi, Wallace Karia kuhusiana na suala hilo alisema,"nipo safarini Arusha kikazi, siwezi kukujibu lolote kwa sasa, hadi nitakaporejea Dar es Salaam."

Simba, Azam hakuna kulala

$
0
0
Sosthenes Nyoni
VITA ya kuwania usukani wa Ligi Kuu Tanzania Bara itaendelea tena leo wakati Simba na Azam watakaposhuka dimbani kuwavaa Kagera Sugar na Tanzania Prisons.

Mabingwa watetezi Simba wanaoongoza ligi hiyo wakiwa na pointi 17, watakuwa nyumbani kwenye Uwanja wa Taifa kuikabili Kagera Sugar, wakati Azam inayoshikilia nafasi ya pili ikiwa na pointi 16, watakuwa kwenye dimba la Sokoine jijini Mbeya kupepetana na Tanzania Prisons.

Tofauti ya pointi moja baina ya timu hizi katika msimamo wa ligi ndiyo iliyoibua mchuano wa aina yake wa kila moja kuhaha kuhakikisha inapigania hadhi yake.

Simba yenye rekodi ya kushinda Dar es Salaam, watashuka katika  mchezo huo wakiwa na kumbukumbu ya kulazimishwa sare 0-0 na Coastal Union, pia watalazimika kucheza kwa tahadhari dhidi ya Kagera Sugar yenye rekodi nzuri katika mechi zake za ugenini ikiwa imepoteza mchezo mmoja pekee walipofungwa 3-2 na Union.

Kocha wa Simba, Milovan Cirkovic anajivunia kurejea kwa winga wake tegemeo Mrisho Ngasa pamoja na kiungo Ramadhan Chombo waliokuwa majerahi.

Pia, huenda Mserbia huyo akamrejesha kwenye kikosi cha kwanza beki Juma Nyoso aliyempumzisha katika pambano dhidi ya Coastal  na kutoa nafasi kwa mara ya kwanza Mkenya Pascal Ochieng kucheza mechi ya Ligi Kuu msimu huu.

Vita kubwa zaidi itakuwa jijini Mbeya wakati wenyeji Prisons watakapokuwa na kazi ya kuepuka kipigo cha pili mfululizo watakapokutana na Azam ambayo haijapoteza mchezo wowote hadi sasa.

Prisons inatajwa kuwa moja ya timu ngumu zinazotumia soka la nguvu na akili wakati wapinzani wao Azam wanasifika kwa soka la pasi fupi fupi, lakini italazimika kutumia mbinu za ziada kwenye Uwanja mbovu wa Sokoine.

Heka heka za ligi hiyo pia zitawashuhudia maafande 'magoigoi' wanaoshikilia mkia Polisi Morogoro wakiwakaribisha JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro.

Mgambo Shooting inayoshika nafasi ya 12 na pointi sita watakuwa wenyeji wa Toto Africans katika pambano litakalopigwa kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga.

Nayo JKT Oljoro iliyojikita katika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi ikiwa na pointi 12 itakuwa nyumbani kwenye dimba na Sheikh Amri Abeid, Arusha kukwaruzana na African Lyon iliyoko katika nafasi ya 13 baada ya kukusanya pointi sita.

TFF yamsaka Nditi wa Chelsea

$
0
0
Jessca Nangawe
SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) linafanya mazunguzo na mabingwa wa Ulaya, Chelsea kupata nafasi ya kumtumia kiungo Adam Nditi katika kikosi cha Taifa Stars na Ngorongoro Heroes.

Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah alisema kufuatia uwezo wa mchezaji huyo kwa sasa wameona ni vema wakafanya mazungumzo na Chelsea ili aweze kuitumikia timu yake ya taifa ya Tanzania.

"Nditi ameonyesha kiwango kizuri katika klabu yake, kama Shirikisho tumeona ni vema tukafanya mazungumzo na Chelsea ili tuweze kumtumia Tanzania,"alisema Osiah.

Mwanzoni mwa mwezi wa Julai, Nditi alisaini mkataba rasmi wa kuwa mchezaji wa kulipwa katika kikosi cha Chelsea kinachofundishwa na kocha Roberto Di Matteo.

Awali Nditi alikuwa akiichezea Chelsea akiwa mwanafunzi mwenye udhamini, lakini sasa timu hiyo inayomilikiwa na tajiri Roman Abramovich imemzawadia mkataba wa kuwa mwanasoka rasmi wa kulipwa katika klabu ya Chelsea inayotumia Uwanja wa Stamford Bridge.

Katika hatua nyingine Osiah alisema kocha wa Taifa Stars, Kim Poulsen anatarajia kwenda nchini DR Congo kuangalia baadhi ya mechi za timu ya TP Mazembe ili kuona viwango vya wachezaji Mbwana Samata na Thomas Ulimwengu.

Osiah alisema uamuzi huo wa kocha Kim kwenda Lubumbashi ni kuangalia nafasi wanazocheza wakiwa na TP Mazembe ili imrahisishie katika kuwatumia Taifa Stars.

"Kocha ataangalia walau mechi mbili watakazocheza Samata na Ulimwengu, lengo ni kutaka kufahamu uwezo na nafasi wanazocheza na kwa nini wakiwa Stars hawachezi katika kiwango cha juu kama wanavyokuwa TP Mazembe," alisema Osiah.

Pia, atazungumza na uongozi wa klabu hiyo kuhusu kuwaruhusu wachezaji hao kuja kuitumikia Taifa Stars anapowahitaji.
Viewing all 166 articles
Browse latest View live